Kuangamiza dhuluma dhidi ya wanawake Waamini wahasiriwa. Chukua hatua sasa!

Get monthly
e-newsletter

Kuangamiza dhuluma dhidi ya wanawake Waamini wahasiriwa. Chukua hatua sasa!

Taarifa ya Layla, Moroko
Afrika Upya: 
24 Novemba 2021
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 

Kati ya wanawake 10  wa dhuluma, ni mmoja pekee atafutaye msaada wa polisi, kimataifa. Lakini aghalabu hata wale wanaoutafuta hatimaye huziondoa kesi kutoka michakato ya haki kwa sababu ya uwajibikiaji mbaya wa askari au washikadau  wengine wa mahakama.

Uwezo wa wanawake kupata haki unaanza kwa kuwaamini wahasiriwa na kuchukua hatua, kila siku.

Kupitia kwa msururu huu wa tahariri maalumu ya Siku 16 za Unaharakati, UN Women inaonyesha sauti za wahaanga na mipango inayoyabadilisha maisha na jamii.

“Aliniambia ananipenda na kwamba alikuwa akipanga kuniposa karibuni. Nilimwamini,” asema Layla Bennani* kuhusu uhusiano wake na mkuu wa kampuni aliyokuwa akiifanyia kazi

 “Ila alinipiga kila tulipotofautiana. Nilivumilia kila kitu, kuanzia dhuluma za kimapenzi hadi kwa jeuri ya kihisia-moyo. Kadri siku zilivyosonga ndivyo alivyoendelea kuwa dhalimu. Alinidhibiti kikamilifu. Alinifanya kuamini kwamba siwezi kumshinda.”

Hatimaye alipoenda kwa askari huku akiandamana na rafikiye, Bi. Bennani hakujua atarajie nini.

“Nilikuwa katika hatua maishani ambapo hapakuwa na jambo muhimu. Nilikuwa mjamzito, sijaolewa, na mpweke. Niliogopa kwamba [askari] wasingeniamini,” afafanua.

 

Layla Bennani amemshika binti yake. Picha: UN Women/Mohammed Bakir.

Kulingana na uchunguzi wa kitaifa 2019 , ni wanawake wahasiriwa wa visa vya dhuluma za kimapenzi 3 pekee kati ya 100 wanaoripoti kwa askari nchini Moroko.

Hofu ya kuaibishwa au kulaumiwa na askari na ukosefu wa imani katika mfumo wa haki inawavunja moyo wanawake wengi kutafuta msaada.

Bi. Bennan alipata kitulizo alipokaribishwa na afisa wa kike wa polisi katika Kitengo cha Polisi wa Wanawake Wahasiriwa wa Dhuluma.

“Jambo la kwanza aliloniambia ni kwamba kuna suluhu kwa kila kitu. Sitawahi kusahau hilo. Imekuwa kaulimbiu yangu maishani. Maneno yake yaninihimiza kumwambia kisa chote. Alinisikiliza kwa makini na uangalifu mkuu.”

Saliha Najeh, chef de police à l'Unité de police de Casablanca pour les femmes victimes de violences. Photo : ONU Femmes/Mohammed Bakir.
Saliha Najeh, Mkuu wa Polisi katika Kitengo cha Polisi cha Casablanca kwa Wahanga wa Ukatili wa Wanawake.. Picha: UN Women/Mohammed Bakir

“Wakati huo sikujihisi salama... kukutana naye kulinifanya kubaini kwamba  nilikuwa na fursa ya kuyakomboa maisha yangu,” Bi. Bennani akumbuka kutagusana mara ya kwanza na Kitengo hicho cha Polisi.

Baadaye Bi. Bennani alielekezwa kwa makao ya kina mama wasio na wenzi wa ndoa alikopata fursa ya pili.

“Binti yangu alizaliwa miaka miwili iliyopita. Yeye ndiye tumaini langu. Jina lake linamaanisha ‘ukinzani’ katika Kiarabu. Hivi maajuzi nilihitimisha shahada yangu katika Hisabati. Nilikuwa nikisoma huku nikimlea binti yangu katika makao hayo ya kina mama wasio na wenzi wa ndoa,” anasema huku akiushika mkono wa mwanawe.

Ni mambo gani yawezeshayo kuangamiza dhuluma za kijinsia

Kuukuza uaminifu na ujasiri katika askari ni sehemu muhimu ya uzuiliwaji wa uhalifu na usalama wa jamii.

Polisi waliopewa mafunzo ya kitaaamu wanapozishughulikia kesi za dhuluma za kijinsia, wahasiriwa wana uwezekano mkuu wa kuripoti dhuluma na kutafuta haki, huduma za kiafya na za kisaikolojia.

Huduma hizi muhimu (essential services) husaidia kuvunja kurudia kwa dhuluma kwa kuwasaidia wahasiriwa, familia na jamii zao kupona, huku zikiwasilisha taarifa muhimu kwa wanawake na jamii kwamba dhuluma kama hizo ni uhalifu wa kuadhibiwa.

Kwa miaka michache iliyopita, Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Kitaifa, akisaidiwa na UN Women na ufadhili kutoka kwa serikali ya Canada, ameifanyia mageuzi idara ya kitaifa ya polisi ili iweze kusaidia wanawake wahasiriwa vyema na kuzuia dhuluma dhidi ya wanawake.

Mwaka 2018, Vitengo vya Polisi wa Wanawake Wahasiriwa wa Dhuluma  katika vituo 132 viliundwa upya.

Mbali na majukumu ya kiupelelezi, vitengo hivyo sasa vinashughulikia uimarishaji wa tajriba ya mitagusano ya awali ya wanawake na polisi kwa kusikiliza, kurekodi, kuandamana na na kuzielekeza kesi. Vituo vyote 444 vya wilaya vya polisi vina wahudumu maalumu wanaowaelekeza wanawake wahasiriwa kwa vitengo vya karibu vya huduma mahususi. 

 Mpango huo wa miaka minne pia umewapa wakuu wa polisi mafunzo na kuondoa vikwazo vingi vilivyowakabili wanawake wahasiriwa. Kwa mfano, wahasiriwa wanaweza kuwasiliana moja kwa moja na Mkuu wa Polisi au wakuu wa vitengo.

“Inahitaji kujitolea kwingi na ujasiri kwa wanawake kuwaomba askari msaada,” asema Saliha Najeh, Mkuu wa Polisi katika Kitengo cha Polisi wa Wanawake Wahasiriwa wa Dhuluma cha Kasablanca.  “Jukumu letu ni kuwapa wahasiriwa muda wote wanaouhitaji kujihisi salama na waliostarehe, na kutuamini kikamilifu ili kusimulia visa vyao.”

Bi. Najeh aliyapata mafunzo maalumu kupitia mpango wa UN Women na sasa anatoa mafunzo kwa maafisa wa askari katika kitengo chake kuhusu namna ya kuzishughulikia kesi za dhuluma za kijinsia, wakitumia mkabala unaompendelea mhanga.  

Jinsi unavyoweza kuchukua hatua
  • Wasikilize wahasiriwa, waelekeze kwa huduma faafu za msaada, na kuza habari zao  kwa kutumia #OrangeTheWorld
  • Fadhili mashirika ya haki za wanawake. Anza kwa kuichukua changamoto #Give25forUNTF25 challenge
  • Ongea. Wape changamoto wanairimu wako kutafakari kuhusu mienendo yao, shutumu maoni ya kibabadume na mienendo, na ongea mtu anapovuka mipaka.

Kufikia mwaka 2021, maafisa wa ngazi za juu wa polisi na wakuu wa vitengo wamepata mafunzo kupitia mpango huo.

Janga la COVID-19 lilipoanza, polisi wa Moroko walikuwa wamejiandaa kuwasaidia wahasiriwa wa dhuluma katika kipindi cha tatizo hilo la kimataifa. Huku huduma nyingine nyingi muhimu zikifungwa, Vitengo vya Polisi wa Wanawake Wahasiriwa wa Dhuluma pamoja na mahakama zilisalia wazi. 

Aidha, Moroko iliongeza mikondo ya wahasiriwa kutoa ripoti na kupata haki kupitia mitandao kwa nambari ya mawasiliano ya bure iliyokuwa wazi saa 24, utaratibu wa kielektroniki wa kutoa malalamishi, na vikao vya mahakama vya mitandaoni.

Kumekuwepo pia juhudi za hivi karibuni kuzifanyia marekebisho sheria za nchi hiyo. Kifungu cha sheria cha Moroko kinaharamisha mahusiano ya kimapenzi nje ya ndoa, hali inayowazuia wanawake ambao hawajaolewa na wahasiriwa wa ubakaji kuripoti dhuluma hizo.

UN Women imesaidia muungano wa mashirika 25 ya wanawake yanayopigania mabadiliko ya sheria hiyo.

Mwafaka wa makubaliano ulioambatishwa kwa mswada na kuwasilishwa bungeni mwaka 2019 na 2020, unalenga kupata ulinzi sawa  wa wahasiriwa wa dhuluma, fasili bayana ya ubakaji, ikiwa ni pamoja na ubakaji katika ndoa, na kuhalalisha mahusiano nje ya ndoa.

*Jina limebadilishwa ili kulinda utambulisho wa mhasiriwa.