AfCFTA yaweza kuinua mamilioni ya wanawake katika uchimbaji wa kiwango kidogo wa madini

Get monthly
e-newsletter

AfCFTA yaweza kuinua mamilioni ya wanawake katika uchimbaji wa kiwango kidogo wa madini

Biashara Huru ya bara Afrika inaweza kubuni mikondo ya maadili na ujuzi kwa manufaa ya wanawake wengi wa Afrika walio katika uchimbaji madini
Afrika Upya: 
6 May 2021
wanawake wakichimba dhahabu
CIFOR/Ollivier Girard
Wanawake hufanya kazi katika wigo zote za operesheni za kuchimba- kwanzia kiwango kidogo haadi kiwango kikubwa. Hao ni wahandisi, majiolojia and wanasayansi lakini wengi wao ni wafanyikazi wa mikono.

Biashara Huru ya bara Afrika inaweza kubuni mikondo ya maadili na ujuzi kwa manufaa ya wanawake wengi wa Afrika walio katika uchimbaji madini.

Nellie Mutemeri
Nellie Mutemeri ni Kiongozi wa Shughuli za Uchimbaji Madini, Mutemeri Consulting na Profesa Mwandamizi, Chuo Kikuu cha Witwatersrand, Johannesburg, Afrika Kusini

Biashara iling’oa nanga chini ya Eneo Huru la Biashara ya Bara Afrika (AfCTA) tarehe 1 Januari 2021 kwa furaha na msisimko. Kulikuwa na sherehe kuu Accra, Ghana, kuliko na usimamizi wa AfCFTA.

Kama Waafrika wengi, nilikuwa na msisimko kuhusu maana ya biashara huru na uhuru  wa kutembea kwa watu katika ya mataifa kwa hali za maisha ya Waafrika walioko katika mataifa 55 ya Umoja wa Afrika (AU).

Kama mwanamke wa Kiafrika ninayefanya kazi katika sekta ya uchimbaji madini, nilijiuliza maana ya AfCFTA kwa mamilioni ya wanawake wachimba madini na wajasiriamali. 

Wanawake wanafanya kazi katika nyanja zote za shughuli za uchimbaji madini—kuanzia shughuli za wasanii na uchimbaji madini wa kiwango kidogo (ASM) hadi kwa uchimbaji madini wa kiwango kikubwa (LSM).  Baadhi ni wahandisi, wanajiolojia na wanasayansi, ila wanawake wengi katika uchimbaji madini ni wafanyakazi wa kazi za sulubu. Karibu asilimia 99 ya wanawake katika uchimbaji madini wamo katika tapo la ASW. Kati ya watu takriban milioni tisa katika ASM katika Afrika, karibu asilimia 50 ni wanawake. Inasikitisha kwamba pia kuna watoto katika ASM.

Katika Afrika, wanawake wanashiriki uzalishwaji wa almasi, dhahabu, johari za rangi, kobalti, shaba, madini maarufu kama 3T (iliyo na madini ya bati, madini ya kutengeneza chuma cha pua na filamenti za taa za umeme pamoja na tantali), madini itumiwayo viwandani na vifaa vya ujenzi, wanazibadilisha baadhi kuwa bidhaa tayari kwa matumizi—kuanzia kwa vyombo vya ufinyanzi na matofali na hata vito. 

Kwa kuzingatia kasi ya uzinduzi wa awamu za mwanzo za AfCFTA na kuondoa ushuru kwa asilimia 90 ya bidhaa zinazozalishwa na mataifa wanachama kunakotarajiwa miaka ya kwanza mitano, ni muhimu kuzingatia, hata katika awamu hii, uwezo wa athari za biashara huru kwa wanawake katika sekta ya uchimbaji madini– haijalishi kama ni chanya au hasi.

Kuangazia athari kama hizo kunaweza kusaidia kubainisha kutimizwa kwa matamanio ya Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya AU  (Africa Mining Vision) (AMV) iliyokubaliwa 2009, na inayopania “kupata uchimbaji wazi, wa usawa na ulioboreshwa wa raslimali za madini na kuhakikisha ukuaji wa uchumi ulio mpana na endelevu pamoja na maendeleo ya kijamii na ya kiuchumi…” na inayotaja ujumuishwaji wa kijinsia kama nguzo zake muhimu, japo utendakazi haujashughulikiwa. 

AfCFTA inawezaje kutimiza au kuimarisha matamanio ya Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya Afrika? 

Ruwaza ya Uchimbaji Madini imekitwa katika uelewa kwamba wanawake wengi katika uchimbaji madini barani afrika wamo katika ASM. Ulimwengu wao ni hatari na uliotawaliwa na ujira mdogo, unyonywaji na mbinu duni za uzalishaji, kutengwa katika mikondo ya thamani, na kadhalika. Hali hii inatokea ilhali inatoa fursa za kutarazaki kwa wanawake wengi katika maeneo ya mashambani.

Inahitaji kuwe na uwazaji unaoongozwa na ushahidi kuhusu madhara kwa mikataba ya kikanda kwa wanawake na hatua zinazohitajika kupunguza athari hizo.

Hapakuwa na mashauriano rasmi na wanawake katika uchimbaji madini wakati wa mchakato uliozalisha AfCFTA.

Huku akiandika kuhusu suala la jinsia na AfCFTA, Fatima Kelleher wa shirika la kuwawezesha wanawake FEMNET (ambalo pia huitwa Mtandao wa Maendeleo na Mawasiliano wa Wanawake wa Afrika) lililoko Nairobi anapendekeza kwamba mkataba huo wa kibiashara uliwachia mataifa husika mzigo mkubwa wa ujumuishwaji wa kijinsia. Hili linatisha kwa kuwa, kihistoria, katika uchimbaji madini, jinsia na ujumuishwaji wa kijamii haujapewa kipaumbele.

Nguzo muhimu za Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya Afrika
  • Kuunda sekta ya madini  ya Afrika iliyo na uanuwai na ushindani wa kimataifa
  • Kuwezesha sekta ya madini iliyo na uwazi na uwajibikaji
  • Kuboresha uelewa na manufaa ya raslimali za madini zisizoundwa upya
  • Kutumia uwezo wa uchimbaji madini kwa kiwango kidogo ili kuimarisha mbinu za kutarazaki na ujumuishwaji katika chumi za mashambani na za kitaifa
  • Kuwezesha maendeeo endelevu yaliyokitwa katika uchimbaji madini unaowajibikia mazingira na jamii
  • Kujenga uwezo wa watu na wa kitaasisi uliokitwa katika uchumi wa maarifa unaosaidia ubunifu, utafiti na maendeleo
  • Kuhakikisha ushiriki wa jamii na raia katika raslimali za madini na ugavi sawa wa manufaa

 

Asili: Umoja wa Afrika

Ili kutathmini uhusiano wa waanawake katika uchimbaji madini na AfCFTA, ni muhimu kuielewa hali ya wanawake katika sekta ya uchimbaji madini.

Masuluhisho yanayopendekezwa 

Ningependa kuona juhudi za makusudi za ujumuishwaji wa kijinsia katika utunzi wa mikataba ya AfCFTA. Hili daima linamaanisha maslahi ya wanawake takriban milioni tano wanaohudumu katika uchimbaji madini barani Afrika sharti yazingatiwe. Kwa hivyo, hatua zifuatazo ni za dharura:

Kwanza, wanawake wanastahili kupigania kuundwa kwa fursa ya kuzingatia shida zao. Fursa zilizomo katika AfCFTA zinaweza kutimizwa tu iwapo vipengele vinavyozingatia ushahidi vimo katika mikataba hiyo. Hivi vinazalishwa vyema katika viwango vya kitaifa na kikanda.

Pili, Mawaziri wa Afrika wa Madini na biashara wanastahili kuuchukua msimamo wa kisera kuhusu uboreshaji wa AfCFTA na Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya Afrika.

Kwa sasa, serikali zinashinikiza unufaishaji na uongezaji thamani wa madini ilhali Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya Afrika inapigania ukuaji wa viwanda unaokitwa katika uchimbaji madini. Lakini hili litawaathiri vipi wanawake wanaohusika katika biashara ya madini barani Afrika? Litakuwa na maana gani kwa madini ambayo mikondo yake ya thamani imeunganishwa kwa mikondo ya kimataifa ya thamani? Na itakuwaje kwa mikondo ya thamani ya kikanda na kuanzishwa kwa viwanda vya kitaifa vya unufaishaji na vya kuongeza thamani?

Tatu, AfCFTA inaweza kupigania matamanio ya Ruwaza ya Uchimbaji Madini ya Afrika pamoja na ujumuishwaji wa kijinsiaa katika sekta ya madini kwa kuhakikisha kwamba mikataba husika ya AfCFTA inafungamana na nguzo muhimu za ruwaza hiyo. Kwa mfano, lengo la AfCFTA “kuendeleza ukuaji wa viwanda, uanuwai wa kiuchumi na kuimarishwa kwa mikondo ya thamani” linatoa fursa ya ushiriki kamilifu wa wanawake kwa manufaa sawa ya mikondo ya thamani ya madini.

Nne, lengo jingine la AfCFTA, ambalo ni “kuweka huru ubadilishanaji wa utoaji huduma” kati ya mataifa, linaweza kupiganiwa huku mataifa yakistawisha mahusiano kuhusu madini ambayo ni muhimu katika mageuzi ya kiuchumi ya Afrika.

Katika kuendeleza ubadilishanaji wa huduma kati ya mataifa, AfCFTA ina fursa ya kupunguza mpaka wa kijinsia katika sekta ya madini.  Kuna haja ya kuweka hatua zinazowezesha usawa wa kupata fursa za kukuza ujuzi, ambao utawahami wanawake watalaamu wachimba madini na wajasiriamali kutoa huduma kama ugunduzi wa madini, mikataba ya uchimbaji madini, na nyingine nyingi.

Mwisho, taratibu za kitaasisi zilizowekwa kuwezesha utekelezwaji wa AfCFTA zinastahili kujumuishwa katika ngazi zote, kulingana na Mkataba wa Maputo (Maputo Protocol to the African Charter on Human and Peoples’ Rights on Rights of Women in Africa).

Ujumbe wangu kwa washirika wa kimaendeleo ni kwao kufahamu usaidizi unaohitajika na wanawake katika sekta ya uchimbaji madini ya Afrika. Kutoa usaidizi huo chini ya mwavuli wa AfCFTA kutauwezesha ujumuishwaji.


Nellie Mutemeri ni Kiongozi wa Shughuli za Uchimbaji Madini, Mutemeri Consulting na Profesa Mwandamizi, Chuo Kikuu cha Witwatersrand, Johannesburg, Afrika Kusini

 

More from this author