Mwongozo wa kutatua changamoto za duniani ni katiba ya UN -Guterres

Get monthly
e-newsletter

Mwongozo wa kutatua changamoto za duniani ni katiba ya UN -Guterres

UN News
25 June 2020
By: 
Wawakilishi kutoka nchi 50 wakiwa kwenye kikao kilichofanyika San Francisco nchini Marekani, kikao kilichofanikisha kuanzishwa kwa Umoja wa mataifa.
UN Photo/Rosenberg
Wawakilishi kutoka nchi 50 wakiwa kwenye kikao kilichofanyika San Francisco nchini Marekani, kikao kilichofanikisha kuanzishwa kwa Umoja wa mataifa.

Katiba ya Umoja wa Mataifa ikiwa inaelekea kutimiza miaka 75 juma hili Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterrres amesema changamoto lukuki zinazoikabili dunia hivi sasa zinahitaji mwongozo ili kuzitatua na mwongozo huo ni katiba ya Umoja wa Mataifa.

Guterres kupitia ujumbe maalum wa maadhimisho ya miaka 75 ya katiba hiyo amesema leo hii dunia inakabiliwa na majanga , na kote duniani watu wanapaza sauti zao dhidi ya ubaguzi wa rangi.

Hata hivyo amesema kukabili changamoto hizo ni mwanzo tu kinachotakiwa ni kuzitatua na dunia ina muda wa kutosha kufanya hivyo kwa pamoja kwa kupitia katiba ya Umoja wa Mataifa "Katiba hiyo ilitiwa sainia miaka 75 iliyopita na misingi yake bado iko hai hii leo ambayo ni imani katika haki za msingi za binanadamu, haki sawa kwa wanaume na wanawake, utu na tahamani ya kila mtu, sheria za kimataifa na utatuzi migogoro kwa njia ya amani, viwango bora vya maisha na uhuru mkubwa. Na maadili haya ya msingi yatatupeleka katika mustakbali mpya.”

Ameongeza kuwa na mustakbali huo ni ule wa kukomesha uharibifu wa mazingira na kuanza kukabili mabadiliko ya tabianchi.

Zaidi ya hapo pia unaopinga ubaguzi na kukumbatia tofauti za ubinadamu, mustakbali ambao vijana wanauongoza mitaani, mashuleni na katika jamii.

Pia Huterres amekumbusha kwamba Umoja wa Mataifa ulizinduliwa kabla ya vitisho kama uhalifu wa mtandaoni na kuibuka kwa kauli za chuki, lakini katiba hiyo inaonyesha jinsi gani dunia inaweza kuzikabili changamoto hizo na hivyo amesisitiza "Hebu na tutambue mtazamo huu wa amani, haki za binadamu na usawa kwa kila mtu, kwa kuungana kwa ubinadamu, umoja na kwa Pamoja.”

Katiba ya Umoja wa Mataifa ilipitishwa rasmi tarehe 26 Juni mwaka 1945 mjini San Fransisco nchini Marekani na ilikuwa kitovu cha kuundwa rasmi kwa Umoja wa Mataifa hapo tarehe 24 Oktoba 1945.

Mada: