Kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa: wakati ni sasa

Get monthly
e-newsletter

Kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa: wakati ni sasa

Viongozi wa dunia katika Mkutano Mkuu wa Hali ya Hewa 2019 wanatarajiwa kuleta mipango halisi ya kupunguza uzalishaji wa gesi chafu.
Franck Kuwonu
Afrika Upya: 
6 August 2019
 South African climate activists. Photo: Ashraf Hendricks /Anadolu Agency/Getty Images
Ashraf Hendricks /Anadolu Agency/Getty Images
South African climate activists.

Athari za mabadiliko ya hali ya hewa zinahisi huko Afrika; nchi, mashirika na watu binafsi, pamoja na vijana, wanachukua hatua za kukabiliana na athari hizi. Katika toleo hili, tunaangazia mipango bora ya hatua ya hali ya hewa na vijana wa Kiafrika.

Madhara mabaya ya mabadiliko ya hali ya hewa, kama vile muda mrefu wa ukame, mioto ya mara kwa mara, upotezaji wa barafu la bahari hadi kuongezeka kwa idadi, muda na nguvu ya dhoruba za kitropiki, zinahisiwa kote duniani kwa kiwango ambacho kinalazimu kuchukuliwa kwa hatua za pamoja kwa haraka.

Mnamo Machi na Aprili, vimbunga vilivuruga mataifa matatu ya Kusini mwa Afrika: Malawi, Msumbiji na Zimbabwe.  Vilisababisha vifo vya mamia ya watu, kujeruhi wengine na kuwafanya maelfu kuhama. Kulingana na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu (OCHA), janga hilo liliathiri zaidi ya watu milioni 1.9 katika eneo hilo, wengi wakihitaji msaada wa kibinadamu.

Katika Pembe la Afrika na Afrika Magharibi, ukame na mafuriko hutokea mara kwa mara na huwa kali. Katika eneo la Sahel, ukame wa muda mrefu unazidisha kuongezeka kwa jangwa, wakati ambapo kuongezeka kwa viwango vya bahari katika miji ya pwani ya Afrika Magharibi, kutoka Ghana hadi Benin, kunaangamiza jamii za wakulima na wavuvi.

Mafuriko katika Asia Kusini yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 100, huku theluji ikionekana katika sehemu za Afrika. Mioto ya mwituni inawaka katika jimbo lote la New South Wales, Australia, nazo dhoruba zinaendelea kushambulia Amerika. Katika bara Ulaya na sehemu tofauti za Amerika, joto limefikia viwango vya juu sana. Hakuna eneo lilio na salama.

Baada ya miaka ya mazungumzo na mijadala, sasa wengi wanakubali kwamba shughuli za kibinadamu, ikiwa ni pamoja na kuchoma mafuta ya fosili, kilimo biashara na ukataji miti, zinapeleka gesi chafu kwenye anga. Gesi hizi huvuta joto kutoka kwa jua, jambo ambalo husababisha joto duniani.

"Ulimwengu unasema ni wakati wa kuchukua hatua," anasema Inger Andersen, Mkurugenzi Mtendaji wa Mpango wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa.

Kulingana na Bi Andersen, hivi sasa ulimwengu unapoteza aina milioni 1 za wanyama na mimea kila mwaka kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa na uchafuzi wa mazingira ambao pia husababisha vifo vya watu wapatao milioni 2.6 duniani kote.

Mkutano wa Mkuu wa Septemba 2019

Mkutano Mkuu wa Hali ya Hewa wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa mwaka 2019 unafuata Mkutano wa Baraza la Mawaziri la Hali ya Hewa Duniani wa Septemba 2018 huko San Francisco na Makubaliano ya Paris kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, ambayo inalazimu pande zote katika makubaliano hayo kuchukua hatua ya kupunguza joto ulimwenguni kwa digrii 1.5 hadi 2 ya sentigredi pekee juu ya viwango vya kabla ya kuasisiwa kwa viwanda. Walihitajika kuwasiliana kufikia 2020 kuhusu mipango yao ya kufikia malengo hayo.

Kwa kuzingatia hayo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ametoa wito kwa viongozi kuja New York mnamo 23 Septemba na mipango madhubuti na ya kweli ya kuimarisha michango yao ya kitaifa kuhusu kukabiliana na hali hii kufikia 2020. Michango ya kitaifa ni mipango ya serikali na inajumuisha malengo yanayohusishwa na hali ya hewa, sera na mikakati ya utekelezaji. Mnamo Oktoba 2018, Jopo la Kimataifa la Mabadiliko ya hali ya hewa lilitoa ripoti maalumu inayoonya waundaji sera kuwa mabadiliko makali ya hali ya hewa yanaweza kuepukwa tu ikiwa mataifa yatatia juhudi za kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa asilimia 45 kutoka viwango vya 2010 ifikapo 2030 na kufanikisha uzalishaji sufuri kwa jumla  kufikia 2050.

Mnamo Septemba 2018, Bw. Guterres aliweka matarajio kwa Mkutano Mkuu wa Hali ya Hewa wa mwaka huu: "Nataka kusikia kuhusu jinsi tutakavyokomesha ongezeko la uzalishaji wa gesi chafu ifikapo 2020, na kupunguza kwa kiasi kikubwa uzalishaji huo kufikia kiwango cha sufuri katika mwaka wa 2050."

Bi. Andersen anaongeza, "Viongozi wa ulimwengu katika mkutano huo wataimairisha ahadi zao, kwa mfano, kuchagua nishati mbadala, kuamua uzalishaji usio na kaboni na kuekeza katika suluhisho za asili kama vile kurejeshwa kwa misitu na ardhi iliyoharibiwa."

Lakini kuna dharura. "Hakuna tena muda wa kupoteza," Bw. Guterres alisema. Viongozi wanapaswa kuja kwenye mkutano "sio tu kutoa taarifa kuhusu kile wanachofanya lakini pia kile wanakusudia kufanya."

Aliorodhesha vitendo vilivyo na uwezo mkubwa wa kupunguza uzalishaji wa gesi chafu na kukuza mabadiliko na uvumilivu, ikiwa ni pamoja na kuongeza kasi ya mabadiliko kutoka kwa mafuta ya fosili kwa nishati mbadala, kutafuta fedha ili kuendeleza matumizi yasiyo na kaboni, kuendeleza juhudi za kimataifa kushughulikia na kudhibiti athari na hatari za mabadiliko ya hali ya hewa, na kuhusisha vijana na umma kwa jumla.

Wakati wa Wiki ya hali ya hewa ya Afrika ya mwaka huu, iliyofanyika huko Accra, Ghana, mnamo Machi, mwakilishi wa YOUNGO, ofisi ya vijana ya Mfumo wa Umoja wa Mataifa juu ya Mabadiliko ya Hali ya hewa (UNFCCC), alibaini kuwa mataifa ya Afrika, ambayo yanachangia kidogo uzalishaji wa gesi chafu duniani kote, yamezingatia michango yao ya kitaifa kuhusu mabadiliko.

Maafa makubwa kama vile vimbunga vya hivi karibuni mara nyingi hunyakua vichwa vya habari; lakini janga lililohusiana na mabadiliko ya hali ya hewa hutokea kila wiki, haswa katika mataifa yanayoendelea, anasema Mami Mizutori, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu kupunguza hatari za majanga. Bi. Mizutori anarudia tena wito wa hatua za kimataifa juu ya mabadiliko ya hali ya hewa katika mahojiano na gazeti la Uingereza, Guardian.

Mkakati wa Kimataifa wa Kupunguza Maafa wa Umoja wa Mataifa (UNDRR) unakadiria kuwa kutoka 1998 hadi 2017, majanga ya mabadiliko ya hali ya hewa duniani yalisababisha hasara ya moja kwa moja ya dola trilioni 2.2 kwa uchumi; majanga mengine yalichangia hasara ya milioni $ 0.7. UNDRR pia inaripoti kwamba barani Afrika, hasara za kiuchumi za majanga ya asili mnamo 2014 peke yake zilikuwa $ 53.19 bilioni.

Wakati wa kuchukua hatua ni sasa

Luis Alfonso de Alba, Mjumbe Maalum wa Umoja wa Mataifa wa Mkutano Mkuu wa hali ya hewa wa 2019, anakumbusha serikali za Kiafrika, asasi za kiraia na sekta ya kibinafsi kwamba wakati wa mazungumzo umekwisha. Ni wakati wa kuchukua hatua, anasema, na kuongeza, "Tunajua la kufanya."

Katika Wiki ya Hali ya Hewa ya Afrika hivi karibuni, viongozi wa Afrika walijitolea kuchukua hatua kuhusu mabadiliko ya hali ya hewa, wakati watu binafsi na jamii ziliwasilisha hatua ambazo tayari walikuwa wanachukua."

"Sisi vijana tunatoa wito kwa serikali zetu kuinua matamanio na kuongeza hatua za hali ya hewa kutuwezesha kufikia malengo yetu," wajumbe wa vijana Zelda Kerubo na Desmond Alugnoa waliuambia mkutano huo katika taarifa ya pamoja.

Kwa kutumia mbinu ya kuchakata tena, uzalishaji na matumizi endelevu, hatua kadhaa, zinazoungwa mkono na mashirika ya misaada ya kimataifa, tayari zinatoa suluhisho endelevu zinazohusiana na matatizo ya hali ya hewa, pamoja na udhibiti wa taka za plastiki, matumizi endelevu ya nishati na kupunguza uzalishaji wa kaboni.

Mpango wa bamboo wa Ghana ni mojawapo ya biashara inayofaulisha uzalishaji na matumizi endelevu. Nchini Uganda, wanafunzi wa Shule ya Upili ya St. Kizito huko Namugongo wanabadilisha taka kuwa mbolea na kuchakata tena plastiki ili kutumika katika sanaa na ufundi (tazama ukurasa wa 6 na 7).  

Ingawa mikakati hii ina athari ndogo kwa ongezeko la joto duniani, ni lazima kuanza mahali fulani, anasema Rukayatu Sanusi, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uvumbuzi wa Hali ya Hewa cha Ghana (GCIC).

GCIC ni mojawapo ya vituo vya uvumbuzi wa hali ya hewa ambacho Kundi la Benki ya Dunia na washirika wake linafadhili kote duniani. Dhamira yake ni kukuza na kusaidia uanzishaji wa biashara za kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa.

"Tunatafuta nia dhabiti kutoka kwa mataifa yanayoendelea katika kuunga mkono miradi inayosaidia viwanda vyao kubuni na kuleta suluhisho mpya kwa maendeleo ya uchumi na uhifadhi wa mazingira," anasema Ganesh Rasagam, Meneja Mtendaji wa GCIC.

Serikali, viwanda na mashirika ya kijamii yana jukumu kubwa katika kushughulikia mabadiliko ya hali ya hewa kama kipaumbele cha maendeleo, kuunda sera sahihi na uwekezaji katika mikakati ya ustahimilivu wa hali ya hewa.

Serikali "ziko mbele na katikati, zikiongoza harakati za kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa," anasema Bwana Guterres.