Kuangazia matumaini na changamoto za vijana wa Algeria

Get monthly
e-newsletter

Kuangazia matumaini na changamoto za vijana wa Algeria

Injaz El Jazair imekuwa ni mshiriki mkuu katika kuwawezesha vijana.
Imène Chikhi
Afrika Upya: 
28 December 2020
Timu ya ITdrops inasherehekea tuzo ya tuzo bora ya bidhaa 2020.
Imène Chikhi
Timu ya ITdrops inasherehekea tuzo ya tuzo bora ya bidhaa 2020.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 
Sauti hii iko kwa Kiingereza.

Injaz El Jazair ni shirika linalojiendesha bila faida nchini Algeria. Lilianzishwa Oktoba 2019 na Bi. Leen Abdel Jaber na limekuwa mshiriki mkuu katika kufundisha vijana kuhusu ujasiriamali, kuajirika  na elimu ya kifedha.

Leen Abdel Jaber, Injaz El Djazair Executive Director.
Leen Abdel Jaber, Injaz El Djazair Mkurugenzi Mtendaji.

Injaz (neno la Kiarabu lenye maana ya kufanikiwa) limeundwa sawa na shirika la kimarekani la vijana, Junior Achievement, ambalo linafanya kazi katika nchi nyingi za Afrika, ikijumuisha Ghana, Nigeria, Tanzania na katika maeneo mengine ulimwenguni.

Lengo kuu la shirika hili ni kuwandaa vijana wa kiafrika kwa ajili ya kufanya kazi katika karne ya 21 ambayo inahitaji wafanyakazi wenye ujuzi katika sekta binafsi na za umma.

Katika kuanzisha shirika hili, Bi. Jaber, ambaye ni mkurugenzi na mzaliwa wa Jordan na sasa anaishi Algeria, alitaka kuwapa vijana barani Afrika fursa ya kukuza ujuzi wao katika uongozi wa biashara, upangaji wa biashara, kufikiria kwa kina na mawasiliano mazuri.

Katikati ya janga la  corona (COVID-19) , ni muhimu kwa vijana nchini Algeria kufikiria juu ya mazingira ya kazi ya siku zijazo na kujiandaa ipasavyo, asema Bi. Jaber, Mkurugenzi Mtendaji wa Injaz El Jazair, katika mahojiano na Afrika Upya.

Ukosefu wa Ajira kwa Vijana

Kuna karibu waalgeria milioni 10.7 wenye umri kati ya miaka 19 na 25, au asilimia 30 ya watu. Kulingana na Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO), licha ya viwango vya juu vya usajili katika taasisi za elimu ya juu-asilimia 51.4, Uwiano wa Jumla wa Usajili (GER) wa mwaka 2018 pamoja na ukweli kwamba kuna idadi kubwa inayoongezeka ya wanawake wanasoma chuo kikuu (asilimia 64.4 GER mwaka 2018), ukosefu wa ajira bado ni changamoto kubwa nchini.

Kiwango cha ukosefu wa ajira mwaka 2019 kilikuwa asilimia 11.4. Inasikitisha, wakati ukosefu wa ajira kwa wanaume ulipungua kutoka asilimia 9.5 kwa mwaka 2018 hadi asilimia 9.1 kwa mwaka 2019, katika kipindi hicho hicho kiwango cha wanawake kiliongezeka kutoka asilimia 19.5 hadi asilimia 20.4

Ukosefu mkubwa wa ajira kwa vijana unadhihirishwa kwa jinsi ambavyo Bi. Jaber anatekeleza mipango yake ya mafunzo. Anaelezea kuwa vijana wengi nchini Algeria hawaongozwi katika taaluma zao na wanakosa kuzifikia jamii za kitaalam ambazo zinaweza kuwaandaa kwa kazi.

Swatech team aiming at providing a technological solution for people with hearing disabilities. Photo: Imène Chikhi
Timu ya Swatech inayolenga kutoa suluhisho la kiteknolojia kwa watu wenye ulemavu wa kusikia. Picha: Imène Chikhi

Vijana wenyewe wana hamu ya kujijengea ujuzi ambao utawawezesha kukidhi mahitaji ya soko la ajira na wanatafuta fursa za kimataifa kupata uzoefu wa kazi, anasema.

Matarajio ya kupata kazi baada ya elimu ya chuo kikuu yalikuwa tayari yamefifia hata kabla ya COVID - 19. Janga hili limezidisha tu hali ya uchumi na athari ya kifedha kwa vijana.

Hata hivyo, kwa kuwa vyuo vikuu vimefungwa, wanafunzi wamepata nafasi ya kushiriki katika mipango mbalimbali ya kujenga ujuzi inayotolewa na mashirika kama Injaz El Jazair.

"Kuwa sehemu ya mtandao wa mafunzo ya ulimwengu, kufikiria mbele na kuwa na mawazo yanayoweza kubadilika kutokana na mazingira ni muhimu kwa wanafunzi na washauri wanaotumia majukwaa ya teknolojia kama Teams katika kufanikiwa kuhudhuria mafunzo ya ujasiriamali mtandaoni wakati wa mfungo- lock down ," asema Bi. Jaber.

Anaelezea zaidi kuwa janga hili limesaidia kuharakisha kujumuisha teknolojia mpya za mafunzo ya umbali, hivyo kupanua ushiriki wa vijana katika programu za mafunzo.

Suluhu zenye ubunifu

Injaz El Jazair pia imetoa tuzo kwa vijana waafrika wenye ubunifu. Kwa mfano, ITdrops, kikundi cha wanafunzi katika Taasisi ya Elektroniki na Uhandisi wa Kielektroniki (IGEE), Boumerdes, Algeria, ikishirikiana na Maabara ya StartUp Lab, ilishinda tuzo ya kwanza katika mashindano yaliyolenga kuleta ufumbuzi katika kupambana na COVID-19. Walishindana na vijana wengine kutoka nchi 13 za Kiarabu, zikijumuisha Bahrain, Misri, Kuwait, Lebanon na Morocco.

Wakiongozwa na mkufunzi wao, Dkt. Dalila Cherifi, wanafunzi walitengeneza kifaa kizuri cha kuzuia maambukizi ya corona wakati wa mfungo-lockdown.

Bi. Jaber pia anajivunia Sawtech (Sawt inamaanisha sauti kwa kiarabu), mradi ulioanzishwa na wanafunzi kutoka Bejaïa, mji wa Mediterania ulioko kaskazini mwa Algeria, ambao wameshiriki katika mafunzo ya ujasiriamali yanayotolewa na shirika lake. Wanafunzi hao wako katika mchakato wa kukuza Akili Bandia ambayo itasaidia watu wenye matatizo ya kusikia na kuongea.

Mafanikio ni barabara ndefu ambayo imejaa vizingiti. Na ni wale tu wanaoshinda vizuizi hivyo watapata mafanikio ya kweli.

Bi. Jaber aliyefurahi asema: "Tulishangaa kuona msaada mdogo kutoka katika shirika letu umewawezesha [wanafunzi wa ITdrops na Sawtech] kufika viwango vingine."

Vijana wana hamu ya kujifunza na hujifunza kwa haraka, anasema, na kuongezeka kwa kasi ya matumizi yao ya mitandao ya kijamii kulitoa fursa ambayo alikuwa tayari kuitumia.

Kwa kuongezea, waalgeria waliopo mijini wanatumia majukwaa mapya ya biashara ya mtandao na huduma za usambazaji, hii inaimarisha matumaini kwa ujasiriamali na fursa za uwekezaji nje ya sekta za jadi za uchimbaji madini, mafuta, na sekta za madini ambazo zinatoa ajira chache kwa vijana.

Siku za zijazo  zenye matumaini

Bi. Jaber ana matumaini kuhusu siku zijazo; anaamini kuwa ujuzi mpya wa kiufundi, uongozi wa biashara na ustadi binafsi utawapa vijana wa Algeria uwezo wa kiuchumi.

Ushauri wake kwa vijana ni "kuwa na ujasiri, uvumilivu na kuazimia kuwa bora kila wakati”.

“Mafanikio ni barabara ndefu ambayo imejaa vizuizi. Na ni wale tu watakaoshinda vizuizi hivi ndio watapata mafanikio ya kweli. ”

Anahitimisha: “Vijana nchini Algeria ni weledi. Wanahitaji kufikiria kuhusu uendelevu wa miradi yao, kuvumilia na kuchukua fursa zote wanazopata. "

Mada: 
Imène Chikhi
More from this author