Biashara huria ya Afrika inaendelea, juhudi zaidi zinahitajika

Get monthly
e-newsletter

Biashara huria ya Afrika inaendelea, juhudi zaidi zinahitajika

Mwaka mzuri watarajiwa AfCFTA inapoadhimisha Miaka 2
Afrika Upya: 
6 January 2023
Presently, intra Africa trade stands low at just 14.4% of total African exports.
Presently, intra Africa trade stands low at just 14.4% of total African exports.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 

Ni mwaka wa pili wa biashara kwenye jukwaa kubwa zaidi la kibiashara barani Afrika – Eneo la Biashara Huria la Bara Afrika (AfCFTA) – na haitakuwa hali ya kawaida katika jumuiya hii kubwa zaidi ya kibiashara ya bara Afrika.

Matarajio ni makubwa na msukumo mpya wa mawaziri wa Afrika unaweza kuwa ndio umetoa msukumo unaohitajika kwa AfCFTA. Pia unatarajiwa kuwa ajenda ya kwanza  katika Mkutano wa Wakuu wa Mataifa na Serikali wa Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa, Ethiopia, mapema mwaka huu.

Kimsingi, mwaka mpya unatoa fursa ya kutafakari kuhusu maendeleo yaliyopatikana, na pia kutazama mbele.

Hadi sasa nchi nane—Kameroon, Misri, Ghana, Kenya, Mauritius, Rwanda, Tanzania na Tunisia—zinashiriki katika Mpango Elekezi wa Biashara wa AfCFTA (GTI), zikiwakilisha kanda tano katika bara zima.

Mpango Elekezi wa Biashara (GTI) ulizinduliwa jijini Accra, Ghana tarehe 7 Oktoba na unalenga kuruhusu ufanyaji biashara muhimu, na kupima mazingira ya sera ya utekelezwaji, kitaasisi, kisheria na biashara chini ya AfCFTA.

“Bidhaa zilizopangwa kuuzwa chini ya mpango huu ni pamoja na vigae vya kauri, betri, chai, kahawa, bidhaa za nyama iliyosindikwa, wanga wa mahindi, sukari, pasta, glukosi, matunda yaliyokaushwa, na nyuzi za mkonge, miongoni mwa nyingine, kulingana na shabaha ya AfCFTA ya kuboresha mkondo wa thamani,” anasema Katibu Mkuu wa Ofisi ya AfCFTA, Wamkele Mene.

Kwa jumla, makadirio ya soko lisilo na mpaka la $ trilioni 3 yanaweza kuwa muhimu katika kubatilisha mwelekeo wa sasa wa umaskini, ukosefu wa usawa na ukuaji katika bara, na kusaidia kuiweka Afrika katika njia ya ukuaji jumuishi na endelevu, inasema UNCTAD katika ripoti yake ya Maendeleo ya Kiuchumi barani Afrika ya 2021.

Novemba mwaka jana, mawaziri wa Afrika waliokutana katika mji mkuu wa Niger, Niamey, walitaka kupitishwa kwa haraka  mapendekezo ya kuongeza kasi ya uanuwai wa kiuchumi, uongezaji thamani, na mageuzi ya kimuundo, ambayo ni sharti la biashara.

"Mkataba wa AfCFTA ulikuwa wa haraka kwani uliepuka changamoto ambapo hakuna kilichokubaliwa hadi kila kitu kikubaliwe," anasema Erastus Mwencha, Naibu mwenyekiti wa zamani wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika (AUC), ambaye alikuwa sehemu ya kikosi kilichotekeleza jukumu muhimu katika uundaji wa jumuiya hiyo ya kibiashara.

"AfCFTA iko kwenye mwelekeo mzuri," Bw. Mwencha anasema, lakini anaongeza: "Kuwa na mkataba wa kibiashara ni jambo moja. Nia njema kisiasa ni jingine kabisa. Ilhali, hicho ndicho AfCFTA inachohitaji zaidi katika hatua hii changa."

Anafafanua kuwa kwa AfCFTA, kazi ilianza pale ambapo kumekuwa na mafanikio huku mazungumzo yakiendelea katika maeneo mengine ambayo maendeleo yamekuwa ya polepole.

AfCFTA iko kwenye mwelekeo mzuri. Kuwa na mkataba wa kibiashara ni jambo moja. Nia njema kisiasa ni jingine kabisa. Ilhali, hicho ndicho AfCFTA inachohitaji zaidi katika hatua hii changa.

Makubaliano ya kuanzisha AfCFTA yalipitishwa tarehe 21 Machi 2018, na 30 Mei 2019 ikaashiria tarehe ya kuanza utekelezwaji wake. Wakati huo, mataifai 24 yalikuwa yamewasilisha hati zao za uidhinishaji. Kufikia Mei 2022 kulikuwa na sahihi 54 ambapo 43 (80%) yalikuwa yamewasilisha hati zao za uidhinishaji.

Ili kusonga mbele, awamu ya utekelezwaji ya AfCFTA ilizinduliwa wakati wa kikao Maalumu cha 12  cha Bunge la Muungano kuhusu AfCFTA huko Niamey, Niger, 7 Julai 2019. Biashara kamili  chini ya Makubaliano ya AfCFTA ilianza tarehe 1 Januari 2021.

Huku ikitajwa kuwa kichochezi cha mageuzi, wataalamu wanadai kuwa AfCFTA imeundwa ipasavyo kuimarisha ushirikiano, kukuza biashara na uwekezaji, kuboresha usafiri wa mitaji na wafanyakazi, kusaidia ukuaji wa viwanda, na ukuzaji wa sekta thabiti ya huduma.

"AfCFTA ni kichochezi cha mageuzi. Kwa AfCFTA, tunaunda bara lisilo na ushuru ambalo linaweza kukuza biashara na uwekezaji katii ya nchi za Afrika, kukuza biashara za ndani, kufufua ukuaji wa viwanda na kubuni ajira kwa vijana wanaoongezeka,” alisema Bw. Mene wakati wa kongamano la ushirikiano wa uwekezaji jijini New York, Septemba mwaka jana.

AfCFTA, alisema, inaipa  Afrika "fursa mpya ya kuelekeza mahusiano yake ya kiuchumi bila kutegemea wafadhili wa nje, wakopeshaji wa kigeni na utegemezi mkuu kwa bidhaa, ikileta enzi mpya ya kiuchumi inayozingatia ushirikiano wa kujitegemea, ushirikiano wa kina na viwango vya juu vya biashara ya ndani ya Afrika”.

Hata hivyo, kuna kazi nyingi mbele

Kwa sasa, biashara ya ndani ya Afrika iko chini kwa asilimia 14.4 tu ya jumla ya mauzo ya nje ya Afrika. Utabiri wa UNCTAD unaonyesha AfCFTA inaweza kukuza biashara ya ndani ya Afrika kwa takriban 33% na kupunguza nakisi ya biashara ya bara hili kwa 51%.

Takriban 34% ya kaya barani Afrika zinaishi chini ya mstari wa kimataifa wa umaskini ($1.9 kwa siku), kulingana na UNCTAD. Wakati huo uo, karibu 40% ya jumla ya utajiri wa bara unamilikiwa na wachache tu.

Kwa hivyo, swali la msingi, AfCFTA inapoadhimisha miaka miwili ya biashara linabaki: Je, ukuaji wa kiuchumi kupitia ushirikiano wa kikanda unawezaje kupunguza umaskini, kupunguza ukosefu wa usawa na kukuza nguzo za maendeleo shirikishi za Ajenda ya 2063 ya AU?

Malengo haya pia yanawiana na Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs) ya kumaliza umaskini uliokithiri (Lengo Na. 1), kuhakikisha usawa wa kijinsia (Lengo Na.5) na kupunguza ukosefu wa usawa (Lengo Na. 10).

Hata hivyo, hata  AfCFTA inapopiga kasi mbele, maendeleo ni ya polepole katika baadhi ya maeneo.

Benin, Gambia na Ushelisheli ndizo nchi pekee za Afrika zinazoruhusu Waafrika wote kuingia bila visa.

Pamoja na hayo, African Development Bank (AfDB) inasema usafiri umekuwa wazi zaidi kwa raia wa Afrika mwaka 2022, na vikwazo vichache.

Sasa kuna mgawanyiko sawa hata kati ya usafiri usiohitaji visa, na usafiri ambapo visa inaweza kupatikana ukifika katika nchi unakoenda, kulingana na Kielelezo cha Uwazi cha Visa cha Afrika cha 2022. Ripoti hiyo ilitolewa na AU na AfDB katika Kongamano la Kiuchumii la Afrika (AEC) la 2022 huko Balaclava, Mauritius.

"Nadhani ni kwelikinzani kwani tunajua kwamba raia wa kigeni wanaweza kuingia na kuzunguka Afrika kwa urahisi zaidi kuliko Waafrika wenzetu," Lamin Barrow, mkuu wa AfDB nchini Nigeria, alinukuliwa akisema pembeni mwa mkutano huo.

"Tunazungumzia enzi ya eneo la biashara huria la bara Afrika. Hivyo, nchi zote za Afrika zinapaswa kufungua mipaka yao kwa Waafrika,” alisema.

Vilevile, Afrika ina 12% ya idadi ya watu duniani, lakini inachukua chini ya 1% ya soko la kimataifa la huduma za angani, kulingana na utafiti wa Benki ya Dunia wa 2010 kuhusu jinsi usafiri huria wa angani ungeweza kuboresha usalama wa angani, kupunguza nauli na kuongezeka kwa trafiki katika Afrika.

AfCFTA ni kichochezi cha mageuzi. Kwa AfCFTA, tunaunda bara lisilo na ushuru ambalo linaweza kukuza biashara na uwekezaji katii ya nchi za Afrika, kukuza biashara za ndani, kufufua ukuaji wa viwanda na kubuni ajira kwa vijana wanaoongezeka.

Anga wazi

Baadhi ya sababu za Afrika kutohudumiwa vizuri, kulingana na utafiti wa Benki ya Dunia unaoitwa “Anga Wazi kwa Afrika—Utekelezaji wa Uamuzi wa Yamoussoukro” ambao unachunguza maendeleo ya Afrika katika kuleta huduma huria  za angani, ni kwamba nchi nyingi za Afrika zinaweka vikwazo kwenye soko la huduma za angani ili kulinda hisa inayomilikiwa na ndege za serikali.

Ili kufikia lengo la 5 la SDG kuhusu usawa wa kijinsia na uwezeshaji wanawake, AfCFTA inahitaji hatua kali za usaidizi zinazolenga wanawake na vijana, ambazo katika baadhi ya mataifa, kulingana na UNCTAD, zinajumuisha takriban 70% hadi 80% ya biashara ndogo ndogo, na wafanyabiashara wafanyao bishara kati ya mataifai; ambao ni sehemu kubwa ya wafanyabiashara wasio rasmi.

Katika jumuiya za kiuchumi za kikanda kama vile Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) na Soko la Pamoja la Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA) biashara rasmi ya kati ya mataifa huchangia hadi 90% ya mtiririko rasmi wa biashara na kuchangia hadi 40% ya jumla ya biashara.

Takwimu za UNCTAD zinaonyesha kuwa uwezo wa sasa wa mauzo ya nje wa Afrika ambao haujatumika unafikia dola bilioni 21.9, sawa na 43% ya mauzo ya nje kati ya mataifa ya Afrika.

Dola bilioni 9.2 za ziada za uwezo wa mauzo ya nje zinaweza kupatikana kupitia uwekaji nusu huria wa ushuru chini ya AfCFTA katika kipindi cha miaka mitano ijayo, linasema shirika hilo la Umoja wa Mataifa.

Kufungulia uwezo

Ili kufungua uwezo ambao haujatumiwa, vikwazo mbalimbali kati ya mataifa ya Afrika visivyo vya ushuru, ikiwa ni pamoja na hatua ghali zisizo za ushuru, mapungufu ya miundombinu, na mapungufu ya taarifa kuhusu soko, vinahitaji kushughulikiwa kwa mafanikio. Hili linahitaji juhudi za pamoja chini ya AfCFTA.

Aidha, ushirikiano wa muda mrefu katika sera za uwekezaji na ushindani utakuwa muhimu. Hili litasaidia kukwepa hali ya wachache kutawala soko na kubatilisha vikwazo vya kimuundo na udhibiti  kuingia sokoni.

Biashara kati ya mataifa ya Afrika inajumuisha 61% ya bidhaa zilizosindikwa na zilizosindikwa nusu, na kupendekeza manufaa ya juu zaidi kutokana na biashaŕa kubwa ya kikanda kwa ukuaji wa kimageuzi na shirikishi, tafiti zinaonyesha.

Tathmini ya Usafiri wa Baharini ya UNCTAD ya 2021 inaonyesha AfCFTA ina uwezo wa kukuza biashara ya baharini barani Afrika, kwani itaongeza utashi wa njia mbalimbali za usafiri.

Kwa upande wake, hii itaongeza hamu ya uwekezaji wa miundombinu, ambayo inafungamana na bandari na vyombo vya baharini.

Miungano ya kikanda ni muhimu kwani unakuza ushirikiano katika ngazi ya kimataifa na kikanda. Inaruka vizuizi vya biashara ambavyo vinazuia usafirishaji wa watu, bidhaa, huduma na utaalamu.

Inaweza kuamua kufaulu au kushindwa kwa AfCFTA.

More from this author