Viongozi wanawake wa Afrika wazindua mpango wa usawa katika kongamano la kihistoria

Get monthly
e-newsletter

Viongozi wanawake wa Afrika wazindua mpango wa usawa katika kongamano la kihistoria

UN News
Afrika Upya: 
14 February 2023
Na: 
African women leaders are playing a key role in transforming the continent. (file)
UN Women/Ryan Brown
African women leaders are playing a key role in transforming the continent. (file)

Hatua za haraka, za pamoja za kuendeleza haki za kijinsia zilijadiliwa katika Kongamano la kwanza la Kimataifa la Uongozi wa Wanawake lililofanyika jijini Juba, Sudan Kusini.

Takribani viongozi 400 wanawake kutoka nchi 15 za Afrika walihudhuria kongamano  la siku tatu liliofadhiliwa na Umoja wa Mataifa, ambalo lilifunguliwa Jumatatu, wakiwemo marais wa zamani na wa sasa.

Lengo ni kusukuma mbele maendeleo, kukabiliana na matatizo na kutafuta suluhisho endelevu kwa masuala yanayowaathiri wanawake na wasichana nchini Sudan Kusini na kote Afrika.

Mada ya kongamano ilikuwa ‘Guwa Ta Mara’, ikimaanisha uwezo wa wanawake.

Katika kongamano hilo, wazungumzaji walikubaliana kwamba changamoto zinaendelea katika uongozi na utawala, mabadiliko ya tabianchi, changamoto za kiuchumi, upatikanaji wa elimu na unyanyasaji wa kijinsia.

"Ulinzi wa haki za wanawake ni muhimu kwetu tulio Serikalini," Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir Mayardit alisema. “Nchi yetu haiwezi kukubali unyanyasaji wa kijinsia, kwani unazuia amani na maendeleo. Tuendelee kufanya kazi tukilenga kuwepo kwa hali bora ya maisha kwa wanawake na wasichana.”

Huku mkataba wa amani wa mwaka 2018 ukiingia katika awamu yake ya mwisho, alisema kuwa Serikali itajitahidi kutatua changamoto zinazowakabili wanawake na kuwawezesha kote nchini.

Juhudi zinazoendelea zinajumuisha kuwapa wanawake fursa ya kukuza ujuzi wao ili kushindana vyema katika soko la ajira.

Tayari Serikali ilikuwa imeongeza asilimia ya uwakilishi wa wanawake kutoka asilimia 25 hadi 35 ,  bighairi ya changamoto za ukosefu wa usalama na ukosefu wa mamlaka zinazowakabili.

"Ingawa hatujafikia kiwango hiki kikamilifu, tutajitahidi ili kutimiza na kuruhusu wanawake kushindana kwa asilimia 65 iliyosalia," alisema Rais Kiir.

'Mahali pazuri pa kuanzia'

“Ushiriki wa wanawake katika mabunge ya Afrika umeongezeka maradufu katika miongo iliyopita, lakini lazima itihada zaidi itiwe,” alisema Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina Mohammed, katika taarifa aliyotoa mbashara kwenye kongamano hilo.

"Mambo mengi yanaendelea kukwamisha uongozi na ushiriki wa wanawake kwa usawa na wenzao wa kiume," alisema, akisisitiza haja ya kuongeza juhudi za kurekebisha hali hii.

"Tunahitaji kuunda vuguvugu la kuleta mabadiliko katika uongozi, na Sudan Kusini ni mahali pazuri pa kuanzia," alisema, na kuahidi kuwa Umoja wa Mataifa ungeunga mkono nchi ya Sudan Kusini katika juhudi zake zinazoendelea na mafanikio ya baadaye. "Tunahitaji wanawake kushiriki katika utafutaji wa suluhisho zinazofaa kwa wote. Kwa pamoja, tunaweza kubadilisha matamanio kuwa vitendo."

Naibu Mwakilishi Maalum wa Umoja wa Mataifa, Sara Beysolow Nyanti alisema uthabiti na azma ya wanawake wa Sudan Kusini unatia moyo.

"Ni matumaini yangu kwamba Sudan Kusini itabadilika na kuwa na amani wanawake wakiwa kwenye mstari wa mbele," alisema, akiongeza kuwa bila ushiriki wao kamili na sawa na uongozi, Sudan Kusini haitasonga mbele katika safari yake kutoka kwenye mizozo hadi amani na maendeleo.

Hata hivyo, changamoto nchini Sudan Kusini bado zinatatiza. Kipaumbele cha juu ni kuongeza uwakilishi wa wanawake katika taasisi za kisiasa na usalama ili kufikia na kuzidi lengo la asilimia 35 lililowekwa katika makubaliano ya amani ya 2018, ambayo yalimaliza vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyodumu kwa muda wa miaka mitano na vilivyosababisha vifo au kuhamishwa kwa mamia ya maelfu ya watu.

Majadiliano pia yatazingatia maandalizi ya uchaguzi wa kwanza wa Sudan Kusini kama nchi huru, unaotarajiwa kufanyika mnamo Disemba 2024.

‘Mikononi Mwao’

Onyesho jipya la video na picha lililoitwa “Mikononi Mwao” liliasisiwa katika kongamano hilo na liliangazia wanawake wanaoongoza juhudi za kueneza amani. Kwa kuakisi mada ya kongamano hilo, nguvu za viongozi wanawake ni nyingi. Wanawake wa Afrika waliwezesha Baraza la Usalama kupitisha azimio muhimu namba 1325 (2000) linalohusu wanawake, amani na usalama, Wanawake wanazidi kutekeleza majukumu muhimu katika kuimarisha amani. Maonyesho hayo pia yanaangazia changamoto zinazowakabili wanawake.

"Vita vimeua matumaini na kugeuza maisha yetu kuwa janga, lakini kazi yangu inanisukuma kuvumilia na kunifanya niwe na matumaini kuhusu siku zijazo,” alisema Olla al Sakkaf, mwanaharakati kijana mwenye umri wa miaka 27 kutoka Yemen, aliyeshuhudia vita vya wenyewe kwa wenyewe vikisababisha uharibifu mkubwa kwa jamii tangu 2014.

"Kila mabadiliko madogo ninayoyaleta katika jamii yangu yananipa matumaini ya maisha bora ya baadaye kwangu na kwa wanawake na vijana kama mimi," alisema.

Alokiir Malual, mwanamke wa pekee aliyetia saini mkataba wa amani wa 2015 nchini Sudan Kusini, pia aliangaziwa katika maonyesho hayo.

"Tunakua," alisema. "Tumetumia mchakato wa amani vizuri, na kuhakikisha mafanikio zaidi kwa wanawake. Tulifikia mgawo wa ushiriki wa asilimia 35 kwa kuungana kama wanawake na kama vikundi, na kuunda masimamo mmoja, dai moja. Mafanikio makubwa ya wanawake wa Sudan Kusini.”