Misusuru ya majadiliano ya Africa Dialogue Series: Kutumia utamaduni kukuza maendelo

Get monthly
e-newsletter

Misusuru ya majadiliano ya Africa Dialogue Series: Kutumia utamaduni kukuza maendelo

Utamaduni tajiri wa Afrika unastahili kwenda zaidi ya mapambo ya kisanii, muziki au densi na kuonyesha mfumo thabiti wa maadili unaoyakumbatia mabadiliko, kukuza ubunifu na kuchangia kwa ulimwengu.
Afrika Upya: 
6 May 2021
Cristina Duarte, UN Under-Secretary-General and Special Adviser on Africa
UN
Cristina Duarte, UN Under-Secretary-General and Special Adviser on Africa

Misururu ya Majadiliano ya Afrika (ADS) 2021 itafanyika katika kipindi kinachokaribiana na Siku ya Afrika inayoadhimishwa tarehe 25 Mei. Kaulimbiu ya mwaka wa 2021 ni “utambulisho wa kiutamaduni na umilikaji: kugeuza mitazamo” na itasherehekea utambulisho, utamaduni, historia na ufanisi wa bara hili kupitia kwa maonyesho na mazungumzo na wasomi wa Afrika pamoja na wataalamu kutoka nyanja mbalimbali, yakiwaleta pamoja washikadau muhimu ili kujadili changamoto na fursa za Afrika, na kwa hivyo kuadhamisha Mwezi wa Mei wa Afrika katika makao makuu ya UN, jijini New York. Bi. Cristina Duarte, Katibu Mkuu Mwandamizi na Mshauri Maalum kuhusu Afrika, anatoa mwangaza kuhusu ile inayoelekea kuwa Misururu ya Majadiliano ya Afrika ya kusisimua:

Misururu ya Majadiliano ya Afrika (ADS) inahusu nini? 

Misururu ya Majadiliano ya Afrika ni jukwaa la utetezi liliotengwa na ofisi ya Mshauri Maalumu wa UN kuhusu Afrika (OSAA) kupigania Afrika na changamoto zake za maendeleo. Zaidi ya hayo, inakusudia kubuni mwelekeo mpya unaoakisi ruwaza ya Afrika kama ilivyowekwa katika Ajenda 2030 na Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika.

Tutarajie nini mwaka huu?

Kaulimbiu ya ADS huchochewa na kaulimbiu ya mwaka ya Umoja wa Afrika (AU). Kaulimbiu ya mwaka huu ni “Sanaa, utamaduni na urithi: nyenzo za kuijenga Afrika Tunayoitaka.” OSAA inaichukulia kaulimbiu hii kutoka kwa mitazamo ya maendeleo na kulenga mbele, huku ikitambua kwamba kuna fursa zinazoweza kutwaliwa kwa kuigeuza mitazamo yetu kabisa baada ya kutatizwa kulikosababishwa na COVID-19.

Hii ndiyo sababu kaulimbiu ya Misururu ya Majadiliano ya Afrika ya mwaka huu ni “Utambulisho wa Utamaduni na umilikaji: kuigeuza mitazamo.” Tunamini kwamba  kaulimbiu ya AU ni wito kwetu kama Waafrika kuirejelea mizizi yetu na roho zetu, kuweka mazingira bora ya kuweka upya na kuamsha upya namna zetu za kufikiria; kuwacha nyuma mitazamo ya kikoloni na ya baada-ukoloni  na kuchukua mitazamo ya kulenga mbele iliyogeuzwa  ambayo itatuwezesha kudhihirisha umilikaji wa hali ya juu.

Una maana gani na kuigeuza mitazamo?

OSAA inapendekeza kuamsha upya namna tunavyowaza kwa kuzingatia mambo matatu: amani, uchumi na mtaji wa binadamu, kupitia kwa vijikaulimbiu vitatu:

Cha kwanza, “Amani Endelevu kwa maendeleo: tukizingatia historia”, inatualika kutazama nyuma katika historia yetu kuelewa na kutafuta masuluhisho kwa mizozo ya sasa. 

Kikaulimbiu cha pili, “Kutumia Utamaduni na Turathi kuleta mageuzi ya kiuchumi,” inaelewa utamaduni kama kiungo muhimu ambacho kinayachangia mageuzi ya kimuundo yanayohitajika mno ya kijamii na kiuchumi, yanayostahili kuanzia ndani ya Afrika, kuathiri uwezo wetu, yakitambua upungufu wetu, kukabili vitu vinavyotutisha na kutwaa kila fursa.

Mahojiano na Cristina Duarte.

Kikaulimbiu cha tatu “Mtaji wa binadamu: utamaduni na turathi kuuwachilia uwezo.” COVID-19 imetufunza kwamba kutoupa kipaumbele mtaji wa binadamu kulikuwa kosa kubwa mno. Katika kujenga mbele vyema na kukomboa kwa wema, tuna fursa ya kulishughulikia suala hili kwa kuweka mtaji wa binadamu katikati ya utungaji sera. Kutoka mtazamo wa utamaduni, hili lina maana, kwa mfano, tunahitaji kupalilia kipengele cha utambulisho miongoni mwa watoto wetu ili wakue watu wazima walio tayari kuudhihirisha umillikaji na uwajibikaji uhitajikao kuukumbatia usasa kutoka ndani.

Sanaa na utamaduni unawezaje kujenga mitazamo ya Waafrika na mielekeo kuhusu Waafrika na ulimwengu wote?

Sanaa na utamaduni hujenga mielekeo na, hatimaye, huathiri namna ulimwengu unavyoitazama Afrika. Tunastahili kwenda zaidi ya dhana finyu ya kuuona utamaduni kama ufundi, upakaji rangi, densi au muziki tu. Hizi ni ishara na taashira za utamaduni wa awali. Ila ukienda katika etimolojia ya neno hili, linamaanisha kupalilia fikra, roho, hivyo vitu vyote dhahania vinavyounda jamii. Kwa mantiki hii, kipengee muhimu zaidi katika utamaduni wetu wa Afrika ni kuwa sehemu ya jamii na kudhihirisha umilikwaji na jamii hiyo.

Kwa karne nyingi sasa, utamaduni wa Afrika umepunguzwa na wakoloni kuwa midhihiriko maridadi ya kisanii. Ni muhimu kutambua thamani ya sanaa na tamadunii za Kiafrika, lakini tunahitaji pia kuelewa –na kuuonyesha ulimwengu—kwamba utamaduni wa Afrika ni zaidi ya mapambo ya kisanii. Pia kwamba ni, kwa hakika, mfumo thabiti wa maadili na uwakilishwaji unaoweza kuyakumbatia mabadiliko, kuchochea ubunifu na ulio tayari kuuchangia uaanuwai wa utamaduni wa ulimwengu kama raslimali muhimu: kutoka kwa mtazamo wa kiutamaduni, hatustahili kuendeleza usare, bali tusherehekee uanuwai wa ulimwengu.

Unahisi vipi kwamba utamaduni unaendesha maendeleo endelevu na fursa ya kupanga upya na kuamsha upya, kama ulivyosema?

Kiini cha utamaduni ni mfumo wa maadili unaofundisha uelewa wa kuwa wa jamii fulani, ambao nao unajumuisha msingi wa maendeleo endelevu. Kwa mfano, nilipokuwa Waziri wa Fedha nchini Cape Verde, nililitekeleza jukumu langu la kisiasa kwa hisia nzito ya kuwa wa jamii ya Wanacape Verde na nikatumia hisia hii kuitumikia jamii yangu. Hili linamhusisha waziri, lakini pia kwa mmiliki wa biashara au mtu mchanga. Maadamu una hisia za kuwa wa utamaduni mmoja unaokufungamanisha wewe na jamii yako, hautakwepa kulipa ushuru, hautaiba mali ya umma, hautaipa jamii yako misimamo mikali na kuishambulia, kwa kuwa utatambua kwamba kila hatua ndogo unayoichukua inaathiri jamii yako. Uhusiano huu kati ya utamaduni na kuwa wa jamii fulani ni sharti la kukubali umilikaji, kukubali jukumu lako katika kuyaendeleza maisha yako, jamii yako na taifa lako. Kwa sababu hiyo utamaduni ni hatua ya kwanza na muhimu katika uongozi unaolenga maendeleo.

Je, janga la COVID-19 limeyaathiri vipi maendeleo katika bara hili, pamoja na utamaduni na turathi?

COVID-19 iliathiri Afrika kwa njia mbalimbali. Athari ya kwanza ilikuwa ya kijamii na kiuchumi. Kabla ya kisa cha kwanza kugunduliwa barani Afrika, bara hili tayari lilikuwa na athari hasi za janga hili kupitia kutatizwa kwa mikondo ya kimataifa ya maadili.  Mshutuko wa pili ulikuwa wakati virusi hivyo vilipofika katika Afrika na serikali zikahitajika kushughulikia athari yake ya kiafya na athari za kijamii na kiuchumi katika hatua za kuvidhibiti.  Tunastahili kukumbuka kwamba mataifa mengi ya Afrika yalikuwa na uwezo mdogo zaidi wa kukabiliana na hali hizi. 

Baada ya miaka 25 ya ukuaji wa imara kidogo wa kiuchumi, Afrika ilikabiiana na  mporomoko wa uchumi na kwa hivyo ukosefu mkubwa wa  raslimali za kukabiliana na janga hili kutoka kwa mkabala wa afya, na pia kushughulikia masuala ya kijamii na kiuchumi. Katika hali hizi, unapokuwa na raslimali chache mno za kifedha, unastahili kuufanya upya ugavi mchungu mno wa matumizi katika bajeti.

Serikali nyingi za Afrika ziliweka nyongeza zaidi za kifedha katika sekta ya afya, huku zikifanya mabadiliko kutoka kwa uwekezaji unaolenga kipindi cha kadri hadi wa kipindi kirefu, kama miundomsingi ya kijamii, kitaasisi na kiuchumi.

Kwa hivyo, kama hatua muhimu hazitachukuliwa kupunguuza pengo lililowachwa katika sehemu hizo, gharama ambayo Afrika itakumbwa nayo kwa kuyafanya haya mabadiliko muhimu ya kipindi kifupi ya ugavi upya katika bajeti itasikika hata zaidi kwa uzito katika miaka ya usoni.

Ni fursa zipi zilizobuniwa na janga la COVID-19 na je, wewe unaonaje uwajibikiaji wa vijana?

Ninafikiri kwamba ni wazi kuwa Afrika ina ubunifu katika DNA yake.  COVID-19 iliunda tu fursa ya uwezo huo kudhihirika. Zaidi ya vipengele 1,000 vya ubunifu wa COVID-19 ulitoka kwa Waafrika, na vijana wamekuwa wabunifu ajabu katika kuwajibikia janga hili. Ninaamini kwamba COVID-19 iliweka fursa ya kutathmini, kwanza, kama tumeyaweka mazingira faafu ya ubunifu, na kama sivyo, ni kitu kipi kinachokosekana katika mkanganyiko huu. Kujenga kuelekea mbele bora hakutawezekana iwapo vipengele hivi vya ubunifu havitazingatiwa daima, kutoka kwa mtazamo wa utungaji sera. Labda tunahitaji kutilia maanani ujenzi wa mifumo ikolojia wa kuuwachilia uwezo wa Afrika kutoka kwa mtazamo wa ubunifu.

Wajibu wa vijana ni upi katika hili?

Vijana wa Afrika wamekuwa wakizitumia sanaa na utamaduni kama mikondo muhimu kuwachilia ubunifu wao. Ubunifu wa COVID-19 ni ushahidi kwamba kwa kweli ubunifu wa vijana Waafrika sio tu midhiihiriko ya usanii maridadi.  Ubunifu wa vijana Waafrika ni raslimali kubwa mno dhahania. Ikiwa utatumiwa vizuri, unaweza kuyachangia mageuzi ya kiuchumi ya Afrika, kwa sababu mageuzi yanahusu ubunifu.  Ukosefu wa mifumo ikolojia kuhusu ubunifu umekuwa ukizizuia jamii kuunganisha na kutumia ubunifu kuendeleza mageuzi ya kiuchumi.

Kutumia AfCFTA

Naamini kwamba Eneo Huru la Biashara ya Afrika (AfCFTA) litaunda soko moja na uwezo wa kuuza bidhaa au huduma kwa wingi kwa sababu ya uwezo mkuu wa uzalishaji, na kwa hivyo kufungulia milango ukuaji wa kiviwanda. Iwapo mifumo ikolojia ya ubunifu itatekelezwa sambamba, huku ikikubalia kizazi kichanga cha Bara Afrika kuwa mshirika mkuu katika kujenga AfCFTA, huenda tukafaulu katika kupiga jeki ubunaji wa nafasi za ajira pamoja na uongezaji imara wa thamani.

More from this author