Hatua ya Tabianchi: Rwanda ni maabara ya mawazo bunifu

Get monthly
e-newsletter

Hatua ya Tabianchi: Rwanda ni maabara ya mawazo bunifu

— Ozonnia Ojielo, UN Resident Coordinator, Rwanda
Kingsley Ighobor
Afrika Upya: 
17 Novemba 2022
LUDOVIC MARIN/AFP via Getty Images
A participant walks past the Rwanda pavillon at the Sharm El Sheikh International Convention Centre, on the first day of the COP27 climate summit, in Egypt's Red Sea resort city of Sharm el-Sheikh, on November 6, 2022

Kama mataifa mengine mengi, Rwanda inaendelea kukumbwa na athari za mabadiliko ya tabianchi, ikiwa ni pamoja na maporomoko ya ardhi na ukame. Serikali na raia, kwa msaada wa UN, wamechukua hatua kadhaa za tabianchi ili kukabiliana na changamoto hizo. Katika mahojiano haya na Kingsley Ighobor wa Africa Renewal katika COP27, Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Rwanda, Ozonnia Ojielo, anaelezea baadhi ya hatua bunifu za tabianchi nchini Rwanda na kuangazia matokeo anayotarajia kutoka COP27. Haya ni madondoo kutoka kwa mahojiano hayo:

Je, tathmini yako kuhusu COP27 kufikia sasa ni gani?

Ilikuwa muhimu kwangu kuhudhuria COP27 kwa sababu maafisa wa serikali ya Rwanda walikuja hapa kwa idadi kubwa, kutokana na wingi wa masuala ya tabianchi ambayo yanawavutia. Na mfumo wa Umoja wa Mataifa unaendana na serikali katika suala la matamanio ya maendeleo. Kwa mtazamo wa Rwanda, umekuwa mkutano mzuri.

Katika siku ya kwanza, Rais Paul Kagame alizindua kituo cha uwekezaji wa kijani kwenye hafla ambayo ilihudhuriwa na watu wengi. Kituo cha uwekezaji kililipwa kupita kiasi—ingawa lengo lilikuwa dola milioni 100, zaidi ya dola milioni 104 zilipatikana katika muda wa dakika 30.

Waziri wa Mazingira [Jeanne d'Arc Mujawamariya] na maafisa wengine wa serikali na wanachama wa mashirika ya kiraia bado wako hapa katika juma la pili. Mazungumzo mengi ya ngazi ya juu yamefanyika, ikiwa ni pamoja na kutiwa saini kwa makubaliano ya hazina ya Michango Iliyoamuliwa Kitaifa (NDCs) na Ujerumani.

Rwanda inatambulika kama kielelezo katika mwitikio wa kitaifa wa athari za mabadiliko ya tabianchi.

Sasa, kwa mtazamo wa Kiafrika au mataifa yanayoendelea, inaonekana kuna kupiga hatua katika masuala muhimu ya ajenda, lakini hatua hizo zinaongezeka. Tunatumai viongozi wetu watajitokeza na suluhisho sahihi.

Afrika haiombi neema kutoka Kaskazini mwa Ulimwengu; Afrika bado inateseka kutokana na historia ya athari za mapinduzi ya viwandani, tokeo la mbinu za maendeleo za Kaskazini mwa Ulimwengu. Bara hili linachangia mgao wa chini zaidi wa utoaji wa gesi hatari duniani lakini linakabiliwa na hatari ya tabianchi. Masuala haya yanahitaji kuzingatiwa katika mazungumzo.

Hatari ya tabianchi sasa nchini Rwanda iko vipi?

Rwanda ni nchi ndogo isiyopakana na bahari. Mara nyingi mimi hutumia neno ‘taifa la mabonde na milima.’ Na hivyo, mafuriko na maporomoko ya ardhi ni changamoto kubwa. Pia kuna changamoto za mfumoikolojia - kutoka ardhioevu hadi vinamasi vya maji.

Serikali ilijaribu kushughulikia masuala haya mapema sana, tangu mwaka 2012 wakati Rais Kagame alipoanzisha hazina ya mazingira, kwa kutambua kwamba taifa halihitaji kuwategemea wengine kuyatatua matatizo yake.

Na kati ya 2012 na sasa [2022], Rwanda imechangisha zaidi ya dola milioni 247 kwa hazina yake hiyo ya mazingirai kuzikabili changamoto hizi. Inatenga ardhi zaidi kwa ajili ya kupiga jeki kilimo, uzalishaji na kukabiliana na maporomoko ya ardhi kupitia kuongezeka kwa ujenzi wa barabara na uimarishaji wa vizuizi vya ardhi na mipaka ya ardhi.

Rwanda imefanya kazi ya kupongezwa kuonyesha kujitolea kwake kwa hatua  ya tabianchi. Uongozi ulikuja kwa COP27 ukiwa tayari kabisa na mpango wa kitaifa kuhusu jinsi ya kupata ufadhili. Taifa hili  lilikuwa miongoni mwa yale ya kwanza kuwasilisha NDC zake zilizofanyiwa marekebisho, ambazo ziligharimu dola bilioni 11, na limejitolea kukusanya karibu nusu ya fedha hizo kutoka kwa rasilimali za nchini huku likitarajia kukusanya fedha zilizosalia kutoka kwa vyanzo vya kimataifa vya ufadhili.

Nchi hiyo pia ilianzisha vituo kadhaa vya kukabiliana na changamoto za tabianchi na ilitekeleza jukumu kubwa katika kazi ya Kikundi cha Wapatanishi wa Kiafrika kuhusu mabadiliko ya tabianchi.

Kwa hivyo, Rwanda inajitolea kwa sababu mabadiliko ya tabianchi yanaliathiri taifa hilo, ingawa mchango wake wa uzalishaji wa gesi hatari ni mdogo mno wa asilimia 0.01.

Je, Umoja wa Mataifa unasaidia vipi juhudi za Rwanda?

Kwa njia nyingi, na lazima niupongeze uongozi wa kisiasa wa Rwanda, akiwemo Rais, Waziri wa Mazingira, na viongozi wa taasisi nyingine muhimu.

Rwanda ina mwelekeo wa serikali nzima wa kushughulikia masuala ya mabadiliko ya tabianchi; inasawazisha maneno na matendo.

Kwa msaada wa Umoja wa Mataifa, taifa liliandaa NDC zake, likiweka mwelekeo ambao serikali na watu wanataka kuchukua. Lilianzisha Mfuko wa Tabianchi wa Kijani. Hazina nyingine zinazohusiana na mabadiliko ya tabianchi zimeanzishwa.

Tuliandaa upya Mfumo wa Ushirikiano Endelevu wa Umoja wa Mataifa ili kuuwezesha mfumo wa Umoja wa Mataifa kuitikia kwa ufanisi zaidi.

Unapotazama mikakati mbalimbali—Mfuko wa Tabianchi wa Kijani, NDC, mipango mbalimbali ya kukabiliana, kumuunga mkono Rais na ushiriki katika COP27—UN imekuwa mshirika wa Rwanda.

Kwa hivyo, katika viwango vya sera, mipango, uratibu na muundo, mfumo wa Umoja wa Mataifa nchini Rwanda umekuwa wa msaada mkubwa.

Vijana nchini Rwanda ni maarufu kwa umahiri wa kiteknolojia. Kwa upande wa hatua za tabianchi, wamekuwa wakifanya nini ambacho vijana katika mataifa mengine wanaweza kutaka kuiga?

Lahaula!

Kuna vitendo vingi vya ubunifu vya vijana wa Rwanda. Youth Connekt Africa,  kwa mfano, ni jukwaa kubwa linaloleta vijana pamoja. Lilianzishwa na Rais wa Rwanda mwaka 2012. Youth Connekt Africa katika mwezi Oktoba mwaka huu lilisherehekea miaka 5 na sasa liko katika mataifa 31 - Nijeria likiwa taifa la hivi punde zaidi kujiunga na kundi hilo.

Ni jukwaa ambapo vijana wa Kiafrika hupata madarasa ya juu, madarasa ya kupalilia ujuzi na mafunzo. Na kisha ufadhili fulani hutolewa. Kuna hazina ya kitaifa ya ubunifu ambayo inaruhusu wale wenye mawazo mazuri kutafuta ufadhili.

Kuna mawazo mengi ya vijana wa Rwanda kuhusu jinsi ya kuweka utaratibu na kurahisisha vifaa vya kilimo kwa ajili ya watu kutumia katika mashamba yao; jinsi unavyowasaidia wakulima kwa kuunda majukwaa ya kujumlisha; jinsi unavyotoa taarifa kuhusu mifumo ya hali ya hewa kwa wakulima; jinsi unavyowaonyesha ufikiaji masoko ili waweze kulinganisha tajriba kwenye bei kwa kutumia rununu zao.

Rwanda ni kama maabara ya mawazo katika Afrika, na mfumo wa Umoja wa Mataifa una furaha kuu kushirikiana na serikali na watu wake, ikiwa ni pamoja na vijana.

Ningewaambia wawekezaji watarajiwa waje Rwanda. Ni ulingo wako kielelezo. Unakuja hapa, unajaribisha, na unaona unafaulu vizuri na unaweza kuongeza.

Pia, Rwanda ni imara kwenye miongozo ya ESG [mazingira, kijamii na utawala] na ni mojawapo ya mataifa yenye viwango vya chini zaidi vya  ufisadi  barani Afrika.

Unapoangalia viwango vya ufanisi wa serikali kote, kwa upande wa mwitikio wa utoaji huduma, imani kwa serikali, usalama, uzingativu wa sheria na kadhalika, tafiti huru zinaituza Rwanda alama za upeo wa 80 na 90 kati ya 100.

Kwa hivyo, ni wakati wa kusisimua kwangu kuongoza juhudi za Umoja wa Mataifa kuunga mkono serikali.

Mwishowe, ni nini kitakufurahisha wakati COP27 itakapokamilika hatimaye?

Naam, kwanza, utambuzi mkuu wa suala la hasara na uharibifu. Tunatumai wataharakisha majadiliano kulihusu na kufikia hitimisho zuri kwa Afrika.

Pili ni suala la ufadhili. Uelewa ni kwamba tunahitaji kuongeza sasa Zaidi ya ufadhili wa kurakibika badala ya kupunguza kwa sababu urakibifu ndio unaoyawezesha mabadiliko kutokea katika maendeleo ya taifa. Ufadhili maradufu wa sasa wa urakibifu ni ombi nadhifu.

Tatu, kuna masuala kuhusu uhamisho wa teknolojia. Urakibifu unahitaji teknolojia, kwa hivyo mijadala ni muhimu kuhusu haki miliki na kuzipa taasisi za Kiafrika haki za umiliki ili kuweza kupitisha na kurakibu teknolojia ambazo zitaimarisha unyumbufu wa tabianchi.

Nne ni mabadiliko ya nishati tu. Tena, sio neema kwa sababu Afrika haikusababisha tatizo hilo.

Kwa hivyo, Ulimwengu wa Kaskazini ulisababisha zaidi changamoto za tabianchi na unastahili kutimiza majukumu yake na kutoa ufadhili kwa Afrika kutimiza usalama wa nishati.

Kama Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alivyosema, kibadala chake ni kuzimu. Kwa hivyo tuushughulikie mshikamano wa kimataifa ili kufanikisha hili kwa Afrika.