Siku 16 za kuhamasisha mapambano dhidi ya ukatili kwa wanawake na wasichana zaanza wadau washauri mambo manne

Get monthly
e-newsletter

Siku 16 za kuhamasisha mapambano dhidi ya ukatili kwa wanawake na wasichana zaanza wadau washauri mambo manne

UN News
Afrika Upya: 
28 Novemba 2022
Na: 
Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia
UN Women/Erica Jacobson
Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia

Leo Novemba 25 kama ilivyo ada ya kila mwaka ni mwanzo wa Siku 16 za kuhamasisha mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na wasichana.  

Mwaka huu, kupitia kampeni ya kimataifa ya Umoja wa Mataifa UNiTE ya kukomesha ukatili dhidi ya wanawake na wasichana, UNiTE, UN Women pamoja na mashirika dada* ya Umoja wa Mataifa wanatoa wito kwa serikali na wadau kuchukua hatua sasa kukomesha unyanyasaji dhidi ya wanawake na kuonyesha mshikamano wao kwa vuguvugu la haki za wanawake na wanaharakati kupitia mambo manne kama ifuatavyo: 

  • Kuongeza ufadhili wa muda mrefu na usaidizi kwa mashirika ya haki za wanawake yanayofanyia kazi masuluhisho madhubuti ya kuzuia na kukabiliana na unyanyasaji dhidi ya wanawake. 
  • Kupinga kurudi nyuma kwa haki za wanawake, paza sauti za watetezi wa haki za binadamu wanawake, na vuguvugu la wanawake wanaotetea haki za wanawake katika utofauti wao na kuhamasisha watendaji zaidi kujiunga na harakati za kukomesha unyanyasaji dhidi ya wanawake na wasichana kote ulimwenguni. 
  • Kukuza uongozi na ushiriki wa wanawake na wasichana katika nafasi za kisiasa, utungaji sera, na maamuzi kutoka ngazi za kimataifa hadi za mitaa, ikiwa ni pamoja na katika michakato ya maendeleo, kibinadamu na amani. 
  • Imarisha taratibu za ulinzi ili kuzuia na kuondoa ukatili, unyanyasaji, vitisho na ubaguzi dhidi ya watetezi wa haki za binadamu wanawake na watetezi/wanaharakati wa haki za wanawake. 

Mashirika dada ya Umoja wa Mataifa, mengine yaliyoshiriki katika wito huu ni pamoja na Idara ya Masuala ya Siasa na Ujenzi wa Amani, Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya kilimo (IFAD), ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, (OHCHR), Mpango wa Uangalizi, Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa Mazingira (UNEP), Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Jinsia na Uwezeshaji Wanawake, Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Dawa za Kulevya na Uhalifu (UNODC), Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu (UNPF), Mtaalam Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu ukatili dhidi ya wanawake na wasichana, sababu na matokeo yake, Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP), na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO). 

UN Women linasema unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana, VAWG ni moja ya dalili mbaya zaidi za ubaguzi dhidi ya wanawake na imesalia kuwa ukiukwaji mkubwa zaidi wa haki za binadamu duniani kote ukiathiri zaidi ya mwanamke 1 kati ya 3, takwimu ambayo haijabadilika kwa kiasi kikubwa muongo uliopita. 

“Kwa mujibu wa  makadirio ya hivi karibuni, zaidi ya wanawake au wasichana 5 huuawa kila saa na mtu wa familia yao.” Inaeleza UN Women.  

Dharura za kimataifa, majanga, na migogoro vimezidisha Unyanyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana, VAWG na kuzidisha vichochezi na sababu za hatari.  

Tangu kuanza kwa COVID-19, asilimia 45 ya wanawake waliripoti kwamba wao au mwanamke wanayemfahamu amepitia aina ya VAWG. Majanga ya asili, ambayo mengi yanawezekana kutokana na mabadiliko ya tabianchi, yanazidisha aina zote za unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana. Hii tayari ilionekana katika miktadha tofauti kama Kimbunga Katrina (2005), tetemeko la ardhi huko Haiti (2010), tetemeko la ardhi huko Christchurch, New Zealand (2011), vimbunga vya kitropiki huko Vanuatu (2011), mawimbi ya joto nchini Uhispania (2008-2016) na moto wa nyikani nchini Australia (2019–2020). 

Katika muktadha wa kupanuka kwa matumizi ya kidijitali kunaokua kwa kasi, ukatili wa mtandaoni dhidi ya wanawake unaowezeshwa na teknolojia unazidisha aina zilizopo za unyanyasaji na kusababisha kuibuka kwa mifumo na aina mpya za Unyanyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana.  

Wakati huo huo, kumekuwa na ongezeko la vuguvugu la kupinga haki, ikiwa ni pamoja na vikundi vya kupinga ufeministi, na kusababisha kupungua kwa nafasi kwa mashirika ya kiraia, upinzani dhidi ya mashirika ya haki za wanawake, na kuongezeka kwa mashambulizi dhidi ya watetezi wa haki za binadamu na wanaharakati wanawake. 

Katika muktadha huu, kukomesha Unyanyanyasaji wa kijinsia dhidi ya wanawake na wasichana kunaweza kuonekana kuwa jambo lisilofikirika, lakini sivyo. Kupungua kwa kiwango kikubwa kwa unyanyasaji dhidi ya wanawake kunaweza kufikiwa kupitia uharakati wa kina wa wanawake na utetezi pamoja na ushahidi na hatua za kisekta mbalimbali zinazofanywa na kutekelekeza uwekezaji.  

Ushahidi unapendekeza kwamba vuguvugu thabiti na linalojitegemea la ufeministi ndilo jambo muhimu zaidi katika kukomesha unyanyasaji dhidi ya wanawake na wasichana.  

Historia ya siku maadhimisho ya leo ya Siku 16 

Wanaharakati wa haki za wanawake wamekuwa wakiadhimisha kila tarehe 25 Novemba kama siku ya kupinga ukatili wa kijinsia tangu mwaka 1981. Tarehe hii ilichaguliwa kuwaenzi akina dada wa Mirabal sisters, wanaharakati watatu wa kisiasa kutoka Jamhuri ya Dominika ambao waliuawa kikatili mwaka 1960 kwa amri ya mtawala wa nchi hiyo, Rafael Trujillo (1930-1961). 

Tarehe 20 Desemba 1993, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha Azimio la Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake kupitia azimio namba 48/104, kuweka njia kuelekea kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na wasichana duniani kote. 

Hatimaye, mnamo tarehe 7 Februari 2000, Baraza Kuu lilipitisha azimio 54/134, likiitaja rasmi tarehe 25 Novemba kuwa siku ya kimataifa ya Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na kwa kufanya hivyo, kukaribisha serikali, mashirika ya kimataifa pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali, NGOs kuungana pamoja na kuandaa shughuli zilizoundwa ili kuongeza uelewa wa umma juu ya suala hilo kila mwaka katika tarehe hii ya 25 Novemba.