Mjumbe Maalum wa AU awahimiza vijana wa Afrika kutumia janga la COVID-19 kuonyesha ubunifu wao

Get monthly
e-newsletter

Mjumbe Maalum wa AU awahimiza vijana wa Afrika kutumia janga la COVID-19 kuonyesha ubunifu wao

28 May 2020
Ms. Ngozi Okonjo-Iweala
Joshua Attah, UA
Mkutano wa Mjumbe Maalum wa AU na vijana

Uwajibikiaji na ukombozi wa janga COVID-19 unatoa fursa kwa vijana wa Afrika kujitokeza na ubunifu katika sekta mbalimbali na hivyo kubuni nafasi zinazohitajika sana za ajira, kulingana Mjumbe Maalum (wa AU) Bi. Okonjo-Iweala.

“Tunaweza kuchagua kuliona janga hili kwa mkabala tofauti kwa kuuliza: ni nafasi zipi zinazoweza kuibuka kutokana na janga hili kwa manufaa ya vijana, hasa ikizingatiwa kwamba ukosefu wa ajira ni tatizo kubwa katika bara Afrika?” aliuliza Bi. Okonjo-Iweala katika majadiliano ya Waafrika mtadaoni tarehe 13 Mei.

“Baadhi ya watu wamevumbua mashine za kidijitali za kufuatilia janga hili … na kuna kila aina za vifaa na teknolojia zinazotumiwa na, kwa mfano Kituo Cha Kudhibiti Magonjwa cha Nijeria (Nigeria CDC), kuchunguza COVID-19.”

Misururu ya mashauriano mtandaoni kuhusu COVID-19: Ukosefu wa Ajira Miongoni mwa Vijana na Ufufuaji wa Uchumi yalifanyika tarehe 13 Mei kwa wenyeji wa Mjumbe wa Masuala ya Vijana wa AU Bi. Aya Chebbi. Bi. Okonjo-Iweala ni mmoja kati ya Wajumbe Maalum wa Umoja wa Afrika (AU) aliyeteuliwa kuandaa msaada wa kimataifa kwa manufaa ya juhudi za Afrika kukabili kusambaratika kwa uchumi kutokana na COVID-19.

Kulingana na Benki ya Dunia, 60% ya wale wasio na ajira barani Afrika ni vijana, na kulingana na Mjumbe Maalumu wa AU, mataifa ya Afrika yanastahili kuwashirikisha vijana katika sekta zote za uchumi ili kuimarisha ubora wa kufanya biashara. Kilimo, alisisitiza, bado ni sekta yenye nafasi nzuri ya kiushindani katika bara hili, “na tunawahitaji vijana kuwazia namna bara hili litakavyojilisha.”

Bi. Okonjo-Iweala alitoa changamoto kwa vijana kujitokeza na teknolojia za kiubunifu za uhifadhi bora wa chakula wakati huu tunaposhuhudia hasara kuu baada ya kuvuna. Katika mataifa yaliyo chini ya Jangwa la Sahara, takwimu za Shirika la Chakula na Kilimo Duniani zinaonyesha kwamba 40% ya hasara baada ya kuvuna na uharibifu wa chakula hutokana na matatizo ya umwagikaji na ukosefu wa uhifadhi bora baada ya kuvuna.

“Hapa ndipo vijana wanastahili kujitokeza na ubunifu wa kuvutia zaidi kuhusu namna tunavyoweza kuhifadhi chakula vyema,” alisema. Lakini ubunifu huu wa kiteknolojia unastahili kuandamana na miundomsingi mizuri, ikiwa ni pamoja na kuwa na teknolojia nzuri ya mawasiliano kama vile viunganishi vya setilaiti.

Haja ya kuwa na uwazi

Washiriki katika majadiliano hayo ya mtandaoni walieleza haja ya serikali kuwa na uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya raslimali za ndani kwa ndani na misaada kutoka nje ya kulikabili janga hili. “Tunataka kuwa na uhakika kuwa pesa zitolewazo zinatumika sawasawa, bali sio tu kuwa na madeni [na hizo pesa] kuingia katika mifuko ya watu,” alisema Admire Mutimurefu wa Zimbabwe.

Bi. Okonjo-Iweala aliwataka vijana kujihusisha katika mipango inayolenga kufuatilia matumizi ya Afrika, kama vile kushirikiana na asasi za kiraia kudai kujua pesa ambazo serikali zinatumia. Wanaweza pia kujitokeza na mbinu za kufuatilia na kuchunguza fedha. “Bara hili ni lenu, ninyi ni 60% ya jumla ya watu wake. Husikeni katika kudai uwazi kutoka kwa viongozi wenu. Bunini, bunini, bunini. Huu ndio wakati,” alisisitiza.

Vivyo hivyo, wataalamu wa teknolojia kama Shikoh Gitau wanaeleza kipindi cha COVID-19 kama kipindi cha kuvutia cha maendeleo ya kiteknolojia cha Afrika, “hasa sasa wakati mipaka yetu imefungwa.”

“Tunaweza kujitegemea wenyewe tu, na kwa hivyo, sisi kama vijana tunastahili kujitokeza na masuluhisho kwa matatizo yetu,” asema Bi Gitau, ambaye ni mwanakamati katika Kamati ya Ushauri ya COVID-19 ya Kenya.